Pages

Monday, January 1, 2018

Jamii imetakiwa kusaidia watoto yatima

Jamii imetakiwa kuweka kipaumbele katika kusaidia watoto yatima, wasiojiweza na  wanaoishi katika mazingira magumu ikiwemo kuwasaidia katika suala zima la elimu pamoja na malazi kwa ujumla.

Wito huo umetolewa jana eneo Sabasaba  jijini Dar es salaam kwenye mkesha wa mwaka mpya  na Kiongozi Prophet Daniel Shillah kutoka kanisa la Bethel International Ministry ambapo amesema kuwa kundi la watu wasiojiweza wanahitaji kupata misaada kutoka kwa jamii inayowazunguka ili wapate furaha.

Aidha Prophet Shillah aliongeza kuwa ni vema kuona umuhimu  na haja ya kuwasaidia ili wapate faraja hivyo na wao kama kanisa wameona umuhimu huo na kutoa mchango wao wa viroba 1000 ambapo vitakua na mchele pamoja na unga wa sembe na kugawa  kwa vituo 20, pia kupitia mchango huo watoto zaidi ya 40  watapata fursa ya kusomeshwa elimu hivyo  kila kituo watoto wawili watapata nafasi hiyo.

''Sisi kama Kanisa sio mara ya kwanza kutoa  misaada  kama hii tumetoa katika vituo mbalimbali ikiwemo salviation army, Temeke, hivyo ni  jukumu letu kufanya hivi kwani tunaona umuhimu wa kusaidia watu wasiojiweza na pia ni fursa kwetu kupata baraka kwa kupitia misaada hii tunayoitoa'' alisema.

No comments:

Post a Comment